YACHAPISHIWE VITABU
Ninabisha ukumbini, mkarimu mhariri,
Nitoe ya fikirani, kwa watu walo mahiri,
Ajitose mhisani, mashairi kuhariri,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Tujitokeze watunzi, wengi tuwe bustani,
Tutoe wetu ujuzi, wa hekima nazo fani,
Tuondoe ya upuzi, tuandike ya maanani,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Ajitoshe mhisani, mashairi kuhariri,
Atazame ukumbini, akusanye mashairi,
Yalo mazito yakini, ya malenga wajasiri,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Wariri wa magazeti, utukufu walojawa,
Wanafasihi tisti, wajuzi wenye vipawa,
Naomba mjizatiti, taji hili kutunukwa,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Washairi wenye fani, kazi zao zaririwe,
Nalikha na Jini Geni, Chokoliti watawazwe,
Naye binti wa Ironi, Jogoo wabarikiwe,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Mbogoli na Chipukizi, pate jinale huko,
Wa pwani naye Chetezi, lako nalo liweko,
Pamoja na Mganguzi, wote wayapate huko,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Na jarida litolewe, lilojawa mashairi,
Na watunzi lichangiwe, ndiyo lipate kunawiri,
Kwa wote linunuliwe, na wapenda mashairi,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Jarida la mashairi, wote kulikimbilia,
Litukuke kwa uzuri, heri ninalitakia,
Yafanyeni mashauri, haya kuyaangalia,
Yachapishiwe vitabu, mashairi yenye sifa.
Naaga kwa tabasamu, nikiwa na tumaini,
Kabla ya huu msimu, tatokea mhisani,
Mwenye huo ukarimu, mwaminifu maishani,
Achapishie vitabu, mashairi yenye sifa.
© Tabu Bin Tabu 2009
